BannerFans.com

MBUNGE SUZAN KIWANGA AKWAMISHA KESI MAHAKAMANI MOROGORO

WIZARA YAWABANIA MAJINA YA VIGOGO KWA KUFUTA AJIRA 200 ZA KONSTEBO NA KOPLO UHAMIAJI.


Katibu Mkuu, Wizara ya Mambo ya Ndani, Mbarak Abdulwakil akizungumza jana kuhusu kufutwa kwa ajira 200 Uhamiaji. Kulia ni Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya jinai nchini (DCI), Isaya Mngulu. Picha na Venance Nestory

Dar es Salaam.
Wizara ya Mambo ya Ndani imefuta ajira 200 za konstebo na koplo katika Idara ya Uhamiaji baada ya kubaini kuwa kulikuwa na upendeleo katika usaili na sasa zitatangazwa upya na kusimamiwa na wizara hiyo.

Akizungumza Dar es Salaam jana, Katibu Mkuu wa wizara hiyo, Mbarak Abdulwakil alisema hatua hiyo imechukuliwa baada ya kamati maalumu ya kuchunguza ajira hizo kubaini wazi kwamba waliopewa nafasi hizo hawakukidhi vigezo.


Abdulwakil alisema wizara imesikitishwa na udhaifu huo baada ya kubainika wazi kwamba malalamiko yaliyotolewa na wananchi na kusababisha wizara kuingilia kati na kufuta usaili wa kuitwa kwenye ajira kwa watu 200 ulikuwa sahihi.


Alisema baada ya kubainika kwamba kweli kulikuwa na upendeleo wa dhahiri kwani watahiniwa wenye sifa na waliopata alama za juu wakati wa usaili hawakuitwa na kukiukwa kwa vigezo vya wazi, ajira hizo zitatangazwa upya na kusimamiwa moja kwa moja na wizara na siyo idara hiyo kama ilivyokuwa awali.


“Kamati hiyo iliyoanza kazi yake Agosti Mosi, mwaka huu ilibaini kwamba hata kigezo cha umri, ambacho ni miaka 25 kwa konstebo na miaka 30 kwa koplo hakikuzingatiwa kwani wenye umri zaidi ya huo waliitwa kazini... “Lakini zaidi, baadhi ya wasailiwa walioitwa kazini ni ndugu na jamaa wa watumishi wa Idara ya Uhamiaji,” alisema.


Alieleza kwamba utaratibu mpya wa kuwapata watu wanaostahili utatangazwa kupitia vyombo vya habari na mamlaka ya usimamizi imerejeshwa kwenye wizara husika badala ya kuachiwa kwenye idara husika.


Alisema pamoja na kwamba miongoni mwa udhaifu uliobainika ni kwamba matangazo ya kazi yaliyotolewa kwenye vyombo vya habari hayakuainisha viwango na madaraja ya ufaulu kwa waliomaliza kidato cha nne na cha sita, lakini hata wale waliofanya vizuri katika usaili hawakuitwa kazini na hakuna sababu maalumu zilizotolewa.


Alisema ajira hizo zilizofutwa zinahusisha pia nafasi 28 zilizokuwa zimetangazwa kupitia Idara ya Uhamiaji Zanzibar.


Alisema si kosa kwa ndugu na jamaa wa watumishi wa Idara ya Uhamiaji kuajiriwa katika nafasi hizo iwapo wanakidhi vigezo vyote, lakini inapotokea kwamba hakuna msimamizi huru ni wazi kwamba kunakuwa na upendeleo kama ilivyotokea na idara hiyo haichukui watumishi kutoka Sekretarieti ya Ajira, kwa kuwa wanaohitajika ni askari.


Ajira hizo zilitangazwa Februari 17, mwaka huu na watu 15,707 walijitokeza kuwania nafasi hizo 200, miongoni mwao, waombaji 1,005 waliitwa kwenye usaili na 200 waliothibitishwa waliitwa kazini.


Hata hivyo, baada ya tangazo la kuitwa kazini malalamiko yaliibuka kupitia vyombo vya habari na baadhi ya mitandao ya kijamii, kwamba baadhi ya walioitwa katika ajira hizo walikuwa ni watoto, jamaa na ndugu wa maofisa wa Idara ya Uhamiaji.


Baada ya kuibuka kwa malalamiko hayo, wizara iliingilia kati na kuunda kamati hiyo ya watu watano Julai 31, ambayo ilipewa siku 10 kukamilisha kazi yake na kutoa matokeo.MWANANCHI
Share on Google Plus

About mtanda blog

Blogger maarufu nchini Tanzania na mwanahabari mkongwe kwenye Tasnia ya habari
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments: