BannerFans.com

MBUNGE SUZAN KIWANGA AKWAMISHA KESI MAHAKAMANI MOROGORO

NAMNA MBUNGE WA JIMBO LA NKASI ALIVYOWATIBUA WABUNGE KUTOKA ZANZIBAR KATIKA BUNGE MAALUMU LA KATIBA MJINI DODOMA.

http://freemedia.co.tz/daima/wp-content/uploads/2014/09/keissy.jpg
MBUNGE wa Nkasi Kaskazini, Ali Keissy (CCM), ‘amechafua hali ya hewa’ bungeni, akisema bila muundo thabiti wa Muungano wa Serikali tatu, Zanzibar itaendelea kuinyonya Tanganyika.


Kauli hiyo ambayo ni kinyume na msimamo wa CCM, inayopigania muundo wa serikali mbili, jana ililitikisa Bunge Maalum la Katiba, ambako wajumbe kutoka Zanzibar walichachamaa wakimvurumishia maneno ya kejeri na kutaka kumpiga, hatua iliyosababisha atolewe ukumbini chini ya ulinzi mkali hadi nje ya eneo la Bunge ili kumnusuru.

Sambamba na tukio hilo, pia wajumbe wengi walipoteza muda mwingi wa mjadala kumshambulia Mwenyekiti wa CHADEMA, Freeman Mbowe, wakisema kuwa hotuba yake ya kutaka kuitisha maandamano ya kupinga Bunge la Katiba ni uchochezi na hivyo kuomba uongozi wa Bunge utoe kauli.

Kama vile sinema, Mbunge wa Mbinga Mashariki, Kapteni mstaafu John Komba (CCM), alisahau kauli yake kwamba atakwenda msituni kupindua Serikali ikiwa muundo wa Serikali tatu utapita, badala yake akamshambulia Mbowe kwamba kauli yake ya kutangaza maandamano na migomo ni kuingilia jukumu la Amiri Jeshi Mkuu kwa kutangaza vita, halafu serikali inakaa kimya.

Licha ya Mwenyekiti wa Bunge hilo, Samuel Sitta kuwabeba dhahiri baadhi ya wajumbe waliyokuwa wakimshambulia Mbowe kwa kuwaacha wazungumze hata baada ya dakika kumi zao kuisha, tukio la Keissy lilionekana kumkera na kuingilia kati kuwapa nafasi baadhi ya makada wa CCM kusafisha hali ya hewa.

ALIVYOANZA KEISSY
Mjumbe huyo ambaye msimamo wake uko wazi kwa kutokubaliana na serikali mbili zinazopigiwa chapuo na chama chake, alianza kwa kumsifu Mwenyekiti wake wa kamati namba moja, Ummy Mwalimu, akisema ni mwanamke jasiri anayefaa kugombea hata urais kwa jinsi alivyowaongoza vizuri.

Hata hivyo, wakati wajumbe wanawake wakimshangilia kwa makofi, Keissy aligeuka na kugusia muundo wa muungano, akisema kwamba huwezi kuzungumza katiba bila kujadili msingi wa muungano ili kuweka bayana ukweli.

“Ukweli lazima uwekwe wazi ili vizazi vijue na kila mtu abebe mzigo wake. Tanganyika imekuwa ikibebeshwa gharama za Zanzibar, tuna wabunge 83 wa Bunge la Jamhuri wanagharamiwa kila kitu wao, wake zao, waume zao familia zao na Serikali ya Tanganyika,” alisema.

Keissy aliongeza kwamba, jambo baya zaidi ni kwa serikali ya Zanzibar kutoweza kuchangia hata senti katika mfuko wa fedha wa pamoja na hivyo kusisitiza kwamba, muungano lazima uwekwe wazi kila mtu agharamie kadiri anavyotumia.

“Hili la Wazanzibari kutochangia gharama za muungano katuambia Gavana Beno Ndullu alipokuja kwenye kamati yetu, sasa tuache kujenga nyumba juu badala ya kuimarisha msingi, huu ni mfumo wa vyama vingi sio kama wakati ule wa chama kimoja wakati wa Nyerere,” alisema.

Alihoji kwamba, hata katika muundo wa serikali mbili unaopendekezwa na CCM, ni vigumu Rais wa Zanzibar kuwa Makamu wa kwanza wa Rais atakayekaimu nafasi endapo rais hayupo, kwani hakuchaguliwa na Watanzania wote.

Hata hivyo, wakati Keissy akiendelea kujenga hoja zake, wajumbe wengi kutoka Zanzibar waliinuka na kuomba kumpa taarifa huku wengine wakiomba mwongozo wa kiti, wakidai mjumbe huyo anapotosha na kuwatusi kwa kauli za kibaguzi.

Keissy alipangua hoja zao hata kabla ya kiti kutoa mwongozo, akiwataka watulie wasubiri amalize huku akisema kwamba, hata.



Bunge hili la Katiba Zanzibar haijachangia, kauli iliyozidisha jazba
wa Wazanzibari wakimwita ‘chizi’ na wengine kudai akapimwe.

“Mimi sio chizi bali machizi ni nyie mnaokubali kubebwa tu bila
kuchangia,” alisema Keissy, kauli ambayo ilimfanya mjumbe mmoja kusimama na kumpa taarifa kwamba muungano umedumisha umoja na kwamba licha ya mbunge huyo kuwa na asili ya Kiarabu ya Pemba bado habaguliwi.

Kabla hata mjumbe huyo kumaliza taarifa yake, Keissy aliendelea tena na kumjibu akisema, asimtukane kwani naye asili yake ni Kongo. Kauli hiyo ilimwinua mjumbe mwingine aliyesema lugha yake inaudhi, inakera na kwamba anapaswa kupimwa akili.

MAKINDA, WASSIRA, HAMAD WAINGILIA
Baada ya hali kuzidi kuwa tete, Spika wa Bunge la Jamhuri, Anne
Makinda, aliomba nafasi kusema neno na kuwataka wajumbe wa Bunge hilo watambue kwamba wamefanya kazi kubwa hadi sasa, hivyo wapuuze yanayojitokeza na kusonga mbele.

Pia, Sitta aliwapa nafasi wajumbe Mohammed Thabit Kombo, Hamad Rashid Mohamed na Waziri Stephen Wassira, ambao walieleza historia ndefu ya muungano, wakisema umeweza kudumu kwa sababu ni wa damu baina ya watu wa pande hizo mbili.

Wassira, alisema kuwa usalama, amani na utulivu ni matunda ya umoja wa watu ambao thamani yake haiwezi kupatikana kwa fedha na hivyo kumshauri Keissy kuchunga kauli zake, akisema ulimi mara zote ndio huzaa matatizo.

Naye Sitta, alisema kuwa ni vigumu kwake kujua mjumbe atazungumza nini, hivyo akawataka kuzingatia kanuni inayolinda majadiliano na kisha akamtaka Keissy kufuta kauli yake kwamba Wazanzibari wanabebwa na Tanganyika.

Katika kuepusha rabsha, muda mfupi baada ya Bunge kuahirishwa kwa ajili ya mapumziko ya mchana, wapambe wa Bunge walimfuata Keissy na kumuondoa ukumbini kijanja, wakimpitisha mlango wa Spika na kumsindikiza hadi nje ya eneo la Bunge.

Hatua hiyo, iliokoa jahazi kwani wajumbe wengi kutoka Zanzibar
walionekana nje ya ukumbi wa Bunge wakimsubiri kwa hamu bila
mafanikio, pasipokujua kwamba alikuwa ametoka nje tayari.

WARIOBA, MBOWE GUMZO
Katika hatua nyingine, hotuba ya Mbowe juzi katika mkutano mkuu wa uchaguzi wa CHADEMA, ya kutaka wafuasi wa vyama vinavyounda kundi la Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA), kuandamana kupinga Bunge hilo kuendelea, imewaumiza wajumbe wengi.

Wajumbe wengi waliochangia wakiwemo Fahami Dovutwa (UPDP), Abdallah Bulembo, Said Nkumba, Boniface Simbachawene, Amos Makalla, Prof. Mark Mwandosya na John Komba (wote CCM), na Maresia Power (201), walisema Mbowe anachochea vurugu.

Wakati Makala akiwaita UKAWA kuwa ni sawa na mtoto deko, Dovutwa alisema kuwa hao hao walimpigia kura Sitta wakidai ni tegemeo la kulinda masilahi yao katika mchakato huo, lakini alivyokataa kufanya hivyo sasa wamemgeuza aduai yao.

Komba alirejea kauli yake ya zamani katika Bunge hilo kwamba,
vurugu zote zinaletwa na Jaji Warioba ambaye anawatuhumu wajumbe wa Bunge hilo kwamba wanakula fedha za wananchi bure wakati tume yake nayo ilikula fedha nyingi.

“Bunge hili litoe tamko kwamba ‘Warioba ni shida’…ni sawa na mtu aliyefufuka kijijini, watu wote wanamkimbia. Alipokuwa ananyolewa…sisi tulikaa kimya, na sisi tunaponyolewa naye akae kimya,” alisema.

Komba alikwenda mbali zaidi na kulishambulia Kanisa Katoliki,
akiwatuhumu maaskofu kwamba wamebadili salamu ya imani ya dhehebu hilo ya ‘Kristu Tumaini letu’ na kwamba wanaagiza waumini waseme; “UKAWA Tumaini letu”.

Augustine Mrema wa TLP, alitumia dakika zake kumi, kuomba CCM wahamie Vunjo ili kumsaidia UKAWA wasimnyang’anye jimbo, na kumtusi Mwenyekiti wa NCCR-Mageuzi, James Mbatia, kuwa aliteuliwa na Rais Jakaya Kikwete wakati havai sketi.TANZANIA DAIMA
Share on Google Plus

About mtanda blog

Blogger maarufu nchini Tanzania na mwanahabari mkongwe kwenye Tasnia ya habari
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments: