BannerFans.com

MBUNGE SUZAN KIWANGA AKWAMISHA KESI MAHAKAMANI MOROGORO

MAKOMANDOO WA JWTZ WANOGESHA SHEREHE ZA MUUNGANO, WAZIRI MKUU MSTAAFU EDWARD LOWASSA ASHINDWA KUHUDHURIA.


Makomandoo wakipita kwa ukakamavu mbele ya Rais Jakaya Kikwete wakati wa kuadhimisha miaka 51 ya Muungano kwenye Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam jana.


Dar es Salaam.
Tanzania jana iliadhimisha miaka 51 ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar huku viongozi wa upinzani wakisusia sherehe hizo za mwisho katika utawala wa Rais Jakaya Kikwete ambazo, makomandoo wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), walitia fora.



Rais Kikwete alikagua gwaride hilo katika sherehe zilizofanyika kwenye Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam na kuhudhuriwa na
viongozi mbalimbali pamoja na maelfu ya wananchi ambao baadhi walilazimika kutumia Uwanja Mkuu wa Taifa kufuatilia shughuli hizo.


Baadhi ya viongozi hao ni pamoja na, Makamu wa Rais, Dk Mohamed Gharib Bilal, Rais wa Zanzibar, Dk Ali Mohamed Shein, Waziri Mkuu Mizengo Pinda, Makamu wa Kwanza wa Rais Zanzibar, Maalim Seif Sharrif Hamad. Wengine ni Rais mstaafu, Benjamin Mkapa, Rais mstaafu wa awamu ya sita wa Zanzibar, Amani Abeid Karume na Waziri Mkuu Mstaafu, Frederick Sumaye.


Wapinzani wasusia
Viongozi wakuu wa vyama vya upinzani hawakushiriki maadhimisho hayo baadhi wakiwa mikoani katika shughuli za kuimarisha vyama vyao kuelekea Uchaguzi Mkuu wa Oktoba.


Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Freeman Mbowe yuko mkoani Kagera na Mwenyekiti wa Chama cha Wananchi (CUF), Profesa Ibrahim Lipumba ambaye yuko mkoani Mtwara.


Hata hivyo, Mwenyekiti wa NCCR-Mageuzi, James Mbatia, Kiongozi wa ACT – Wazalendo, Zitto Kabwe hawakuhudhuria na sababu za kutokuwapo kwao hazikuelezwa.


Wakuu waliokosekana
Pia, baadhi ya viongozi wa kitaifa hawakuonekana katika sherehe hizo akiwamo Rais mstaafu wa awamu ya pili, Ali Hassan Mwinyi, Mawaziri wakuu wa zamani, Jaji Joseph Sinde Warioba, John Malecela, Salim Ahmed Salim, Cleopa Msuya na Edward Lowassa.


Kikwete uwanjani
Kama ilivyo kawaida, msafara wa Rais Kikwete aliyekuwa na Mkuu wa Majeshi, Davis Mwamunyange katika gari maalumu la jeshi lililozungukwa na magari mengine saba na pikipiki 15, ulizunguka uwanja huku kiongozi huyo akipunga mkono na kushangiliwa kwa nguvu.


Hatua hiyo ilifuatiwa na wimbo wa Taifa sambamba na mizinga 21 na kisha Rais Kikwete ambaye pia ni Amiri Jeshi Mkuu alikagua gwaride la vikosi vya ulinzi na usalama.


Hata hivyo, wakati akikagua gwaride hilo, Rais Kikwete alipofika kwenye Kikosi cha Bendera, alisahau kupokea heshima hali iliyomfanya arudi nyuma kufanya hivyo kisha kuendelea kukagua vikosi vingine.


Baada ya hapo, ndege za kivita zilipita juu ya uwanja zikitokea Kaskazini kulekea Kusini mwa uwanja. Tukio hilo liliwafanya wananchi waliofurika katika uwanja huo kushangilia hasa kwa jinsi ndege hizo kivita zilivyokuwa zikifanya madoido angani.


Ndege hizo zilifuatiwa na gwaride la nje lililokuwa na vikosi 13 vikiongozwa na bendera ya Rais na ile ya JWTZ zilizokuwa sambamba na bendera saba, sita zikiwa ni za vikosi vya majeshi ya ulinzi na usalama pamoja na ya kikundi cha usindikizaji. Vilipita mbele ya Rais kwa mwendo wa haraka. Baadaye Vilifuata vikosi viwili; Kikosi Maalumu cha Wanamaji (Marine Special Force) na makomandoo vikiwa katika mwendo wa mchakamchaka.


Baada ya makomandoo kupita, alifuata askari polisi mmoja wa jeshi (MP) aliyepita peke yake kwa mwendo wa ‘digidigi’ na kushangiliwa kwa nguvu.


Makomandoo
Sherehe hizo zilikuwa na mvuto wa aina yake kutokana na manjonjo ya makomandoo hao walipokuwa wakipita mbele ya Rais Kikwete.


Kikosi cha makomandoo hao kikiwa katika mavazi ya kivita, bunduki, mabegi mgongoni hukuwa wakiwa wamepaka rangi nyuso zao, waliingia huku wakikimbia mchakamchaka na kushangiliwa kwa nguvu.


Halaiki
Sambamba na makomandoo, halaiki ya watoto iliyoonyesha mafunzo katika meli ya kivita nayo iliwanyanyua wananchi katika viti vyao kushangilia huku waliokaa jukwaa kuu wakiinua bendera na kuzipepea.


Halaiki hiyo iliyoingia uwanjani saa 5.10 ilianza kwa kutoa ujumbe wa sherehe hizo kwa mwaka huu ambao ni “Miaka 51 ya Muungano, Tudumishe Amani na Umoja, Ipigie Kura ya Ndiyo Katiba Inayopendekezwa na Kushiriki Uchaguzi Mkuu.” Kisha kuhamasisha kilimo wakisisitiza matumizi ya zana za kisasa. Pia, watoto hao wa halaiki walitoa ujumbe kupinga ujangili katika mbuga za wanyama ili kulinda maliasili hiyo kwa ajili ya vizazi vijavyo. Kadhalika, walihamasisha ujasiriamali wa kutumia kazi za mikono.


Kivutio kikubwa katika halaiki hiyo ilikuwa ni jinsi watoto hao walivyohamasisha ulinzi ambako walitoa ujumbe kuwa suala hilo ni jukumu la wananchi wote. Wakati wanatoa ujumbe huo walikuwa katika mwendo wa haraka huku wakienda mbele na nyuma na kutoa burudani nzuri kwa hadhira iliyokuwepo uwanjani hapo pamoja na watazamaji kupitia runinga.


Wakiendelea na onyesho la ulinzi, watoto hao walipita katika vikwazo huku wakiruka na kupita katikati ya maduara makubwa ya vyuma yaliyokuwa yanawaka moto na kisha kukanyaga makarai yaliyokuwa na moto pia.


Pia kulikuwa na watoto watatu waliopita juu ya kamba kwa staili tofauti na kuwavutia wazazi waliokuwapo. Wa kwanza alipita huku akining’inia kwa mikono yake. Alifuatiwa na aliyeshika kamba kwa mikono pamoja na miguu; uso ukielekezwa angani. Wa mwisho alipita juu ya kamba hiyo kwa kutambaa.


Mazoezi mengine ni yake ya mfano wa meli ya kivita yaliyokuwa yameandaliwa kwa umakini mkubwa. Watoto hao walipanda mnara wa meli hiyo kwa aina tofauti. Kuna aliyepanda kwa mikono pasipo miguu yake kugusa nguzo. Mwingine alipanda huku miguu yake ikiwa imenyooka mbele na wa mwisho alipanda kwa kuruka ruka.


Wakiwa bado ndani ya meli hiyo, mmoja alijifunga kamba mguuni na kuwanyanyua wenzake wawili kutoka chini. Ilikuwa ni mithili ya filamu nzuri ya kivita.


Kabla hawajaondoka, walipita katika mfumo wa vifaru vya kivita. Kimoja kikiwa cha kupiga masafa marefu na kingine mafupi. Watoto watatu walitengeneza matairi ya vifaru hivyo. Usingependa kuondoka wala kutaka watoto hao wamalize kuburudisha. Kwa hakika walivutia.


Ngoma, Kwaya
Baada ya halaiki zilifuata ngoma za makabila. Ngoma nne zilitumbuiza, mbili kutoka visiwani na nyingine bara. Pia kwaya kutoka Chunya, Mbeya ambayo ilifuatiwa na wimbo maalumu.


Wapongeza


Akizungumzia sherehe hizo, Spika wa zamani wa Bunge, Pius Msekwa alisema kudumu kwa Muungano ni suala la kujivunia kwani yapo mataifa mengine yaliyoshindwa.


“Tumepita katika mawimbi makubwa au kero za Muungano huu. Ingawa tumefanikiwa kuyavuka lakini ukweli ni kwamba yametuyumbisha sana. Ninaandika kitabu ambacho kinazungumzia historia ya Muungano tangu tulipouanzisha,” alisema Msekwa.


Alitoa mfano wa mataifa yaliyojaribu kuungana na kushindwa kuwa ni Senegal na Gambia; Malaysia na Singapore.


Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Mwalimu Nyerere, Joseph Butiku alisisitiza vijana kujitokeza kwa wingi na kushiriki katika Uchaguzi Mkuu ujao.


Mwenyekiti wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), Jaji Damian Lubuva alisema: “Nakumbuka sherehe za Muungano za mwaka 1977 niliteuliwa kuwa Mwanasheria Mkuu wa Zanzibar na tangu hapo nimekuwa nikiitumikia Serikali. Ni siku ya kumbukumbu yangu muhimu katika maisha na taaluma pia,” alisema Jaji Lubuva.


Awali
Kabla ya sherehe hizo kuanza, milango ya Uwanja wa Uhuru ilifunguliwa saa 12.30 asubuhi na wananchi kutoka maeneo mbalimbali ya jiji kuanza kuingia. Mpaka inatimu saa 2.00 asubuhi uwanja huo ulikuwa umejaa na wananchi kulazimika kuingia Uwanja wa Taifa.MWANANCHI
Share on Google Plus

About mtanda blog

Blogger maarufu nchini Tanzania na mwanahabari mkongwe kwenye Tasnia ya habari
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments: