BannerFans.com

MBUNGE SUZAN KIWANGA AKWAMISHA KESI MAHAKAMANI MOROGORO

RED BRIGADE WA CHADEMA WAKAMATWA NA SARE ZA JESHI NA SILAHA ZA JADI MBEYA.

 

JESHI la Polisi mkoani Mbeya linawashikilia watu wawili wanaodaiwa kuwa makada wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) ambao ni vijana wa kikosi cha ulinzi cha chama hicho (Red Brigade), wakidaiwa kuwa na sare za jeshi na silaha zikiwamo za jadi.

Akizungumza na waandishi wa habari mjini hapa jana, Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Mbeya, Ahmed Msangi, alisema vijana hao walikamatwa juzi jioni katika eneo la Sogea wilayani Momba, baada ya kutolewa taarifa na raia wema.

Kamanda Msangi aliwataha vijana hao waliotiwa mbaroni kuwa ni Mathayo Mwafongo na Salehe Sichalwe, ambao kwa pamoja walikutwa na visu, manati, mawe ya kurushwa kwa kutumia manati, sare za jeshi na simu tatu za mkononi.

Vijana hao pia walikuwa na fulana ya Chadema, kilemba na barua tatu za kuwatambulisha kuwa wao ni wafuasi wa Chadema waliokuwa wakienda Kata ya Chitete, Msangano na Kamsamba wilayani Momba, kutoa mafunzo kwa vijana wa chama hicho.

Kamanda Msangi alisema kutokana na kushamiri kwa matukio ya ugaidi katika maeneo mbalimbali, jeshi la polisi limeweka ulinzi kudhibiti matukio hayo katika kila kona ya nchi.

“Kwa hiyo wakati askari wakiwa katika doria, walipata taarifa juu ya watu hao na kuzifanyia kazi,” alisema Msangi.

Alisema askari wa doria kwa kushirikiana na wananchi, waliweza kuwakamata vijana hao saa tatu asubuhi wakiwa kwenye pikipiki.

Kamanda alisema vijana hao walikamtwa eneo la Sogea, Tunduma wakiwa wamevaa mavazi meusi, wamebeba mikoba mgongoni na wakiwa wamefunika nyuso zao.

“Raia wema walifika kituoni na kutoa taarifa juu ya hofu yao kwa watu hawa ambao walikuwa wamevaa mavazi tofauti na muonekana wa watu wengine…tulivyowafuatilia tuliwakamata na walipopekuliwa walikutwa na silaha na sare za jeshi.

“Hivi sasa wanahojiwa na polisi na mamlaka nyingine kufahamu lengo la kumiliki vitu hivyo kinyume cha taratibu, baadaye watafikishwa mahakamani,” alisema Msangi.

Kamanda wa Ulinzi Chadema Nyanda za Juu Kusini, Aron Siwale alikiri kumtambua mtuhumiwa Mathayo Mwafongo huku akimkana Salehe na kusema kuwa ni dereva wa bodaboda.

MBOWE
Akizungumzia tukio hilo, Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe, amedai chama chake kinawindwa na polisi kila kona.

Kauli hiyo aliitoa jana alipozungumza na MTANZANIA akisema kuwa polisi wamekuwa na kazi kubwa ya kuhakikisha kikosi cha ulinzi cha Red Bregade hakifanikishi malengo yake.

“Tunawindwa kila kona ya nchi hii, polisi hawalali kwa ajili yetu sisi…nawaambia tutakufa nao katika hili, haturudi nyuma,” alisema Mbowe.
Share on Google Plus

About mtanda blog

Blogger maarufu nchini Tanzania na mwanahabari mkongwe kwenye Tasnia ya habari
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments: