BannerFans.com

MBUNGE SUZAN KIWANGA AKWAMISHA KESI MAHAKAMANI MOROGORO

RAIS JAKAYA KIKWETE ABEBA KERO ZA MADEREVA MGONGONI, AAGIZA SUMATRA IMPELEKEE RIPOTI MOJA KWA MOJA IKULU.

Dereva wa basi la abiria, Nusra Maguluko akiwa kazini wakati akifanya kazi katika mpuni ya mabasi ya SHABIBY LINE yanayosafirisha abiria kati ya mkoa wa DODOMA na DAR ES SALAAM.

RAIS Jakaya Kikwete ameagiza kero za madereva nchini, zianze kutatuliwa na ripoti za hatua zitakazoanza kuchukuliwa kuanzia kesho, zipelekwe kwake moja kwa moja. 

Amesema hayo jana alipokutana na wanachama wa Chama kipya cha Madereva (TADWU), wakati alipokutana nao jijini Dar es Salaam akiwa na maofisa wa Wizara ya Kazi na Ajira, Kikosi cha Usalama Barabarani na Mdhibiti wa Usafiri wa Majini na Nchi Kavu (Sumatra). http://www.mwananchi.co.tz/image/view/-/2897896/highRes/1137171/-/maxw/600/-/124yve1/-/pic+jk.jpgRais Jakaya Kikwete, akizungumza na madereva katika mkutano uliondaliwa na Chama Cha Wafanyakazi Madereva Tanzania (TADWU), uliofanyika Dar es Salaam jana. 

Akizungumza katika mkutano huo baada ya kupokea risala ya madereva hao, Rais Kikwete aliagiza Sumatra kumpa taarifa ya namna walivyojipanga kukagua madereva wenye mikataba na wasio na mikataba.

"Jumatatu lazima mnipe taarifa ya mkutano wenu, Sumatra kwenye hiyo mikataba mnahakiki nini na nani ana mkataba na nani hana mkataba," alisema Rais Kikwete. 


Rais Kikwete aliwataka Sumatra pia kusimamia mazungumzo kati ya wamiliki wa magari na madereva na kupata muafaka katika matatizo ambayo yamekuwa yakilalamikiwa na madereva hao kwa muda mrefu bila ufumbuzi hasa katika masuala ya posho na mishahara.

"Mikataba ambayo inaonesha mtu analipwa kiasi gani na posho yake ni kiasi gani hiyo ndiyo mikataba kamili, hata mimi nilipoingia, nilipewa mkataba unaoeleza kwa miaka mitano Rais unastahili hiki na hiki," alisema Rais Kikwete. 


Rais Kikwete alisema hana mamlaka ya kupanga posho lakini aliwataka Sumatra kukaa chini na wamiliki wa magari, madereva na Wizara ya Kazi na Ajira kupanga namna ya kuwalipa madereva.

"Mnapotegemewa kusimamia na hamsimamii vizuri mnatengeneza manung'uniko... tendeni haki, simamieni vizuri," alisema Rais Kikwete. 


Awali Mkurugenzi Mkuu wa Sumatra, Giliad Ngewe aliwekwa katika wakati mgumu na Rais Kikwete baada ya kuulizwa maswali ni lini wanapitia mikataba ya madereva hao, ambapo alijibu kwa kusua sua jambo lililofanya madereva waliojaa katika ukumbi huo kumzomea.

Rais Kikwete alibaini kuwa madereva wengi hawana mikataba jambo lililosababisha wafanye kazi katika mazingira magumu ambapo aliwataka Sumatra kuhakikisha madereva wote wana mikataba. 


Alisema sekta ya usafirishaji inachangia kwa kiasi kikubwa katika ukuaji wa uchumi wa nchi na madereva ndio wanaoendesha uchumi wa nchi.

Kuhusu madai ya madereva kupigwa tochi na askari wa usalama barabarani wawapo safarini, aliwataka madereva hao kutii sheria sambamba na kuzingatia sheria za usalama barabarani. 


Alisema madereva nao wamekuwa wakikiuka sheria za barabarani na kusababisha ajali nyingi zinazotokea nchini na kusababisha maafa makubwa na upotevu wa mali. 

Rais Kikwete alitoa mfano wa alama za barabarani zinazoonesha kuwa dereva hapaswi kwenda kwa kasi ya zaidi ya kilometa 80 kwa saa, lakini unakuta dereva ndio anakanyagia kasi ya kilometa 120 kwa saa.

Alisema kama madereva wangekuwa wakitii sheria na alama za barabarani, kusingekuwa na haja ya hizo tochi, lakini vifaa hivyo vinawekwa kutokana na madereva kutotii sheria. 


Mbali na hayo, Rais Kikwete pia aligusia suala la kuzidisha mizigo katika magari na kusema madereva wamekuwa wakipewa uzito maalumu wa mizigo yao, lakini wanazidisha, hata hivyo madereva hao walipiga kelele kuwa ni tatizo la wamiliki. 

Mpinga na Matrafiki
Hata hivyo, alimtaka Kamanda wa Kikosi cha Usalama Barabarani, Mohamed Mpinga, kuondoa matrafiki wanaoomba rushwa barabarani. 


Alisema madereva wa nje ya nchi wanaobeba mizigo kutoka Bandari ya Dar es Salaam kwenda katika nchi zao, wamewaeleza viongozi wao kuwa wamekuwa wakilazimika kuwa na bajeti ya rushwa wanazoombwa na trafiki barabarani. 

Aliwapongeza madereva kwa kuanzisha chama cha kuweka na kukopa na kusema kuwa naye atawasaidia.

Kuhusu mafunzo, alimuagiza Kamanda Mpinga kutafuta namna ya kuzungumza na wamiliki wa magari, ili mafunzo hayo ya kila baada ya miaka mitatu, yafanyike kwa utaratibu utakaotunza ajira za madereva na gharama zilipwe na wamiliki.HABARILEO
Share on Google Plus

About mtanda blog

Blogger maarufu nchini Tanzania na mwanahabari mkongwe kwenye Tasnia ya habari
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments: