BannerFans.com

MBUNGE SUZAN KIWANGA AKWAMISHA KESI MAHAKAMANI MOROGORO

MWILI WA MWENYEKITI WA CHADEMA MKOA WA GEITA ALPHONCE MAWAZO SASA KUAGWA RASMI LEO BAADA YA KUMALIZIKA KWA KESI KATIKA MAHAKAMA KUU KANDA YA MWANZA.

ALIYEKUWA Mwenyekiti wa Chadema mkoa wa Geita, Alphonce Mawazo enzi za uhai wake.

Mwanza. Hatimaye amri iliyowekwa na Jeshi la Polisi Mkoa wa Mwanza ya kuzuia shughuli ya kuaga mwili wa aliyekuwa Mwenyekiti wa Chadema mkoa wa Geita, Alphonce Mawazo imetenguliwa na Mahakama Kuu Kanda ya Mwanza, sasa ataagwa kwa heshima zote jijini hapa.

Kufuatia hukumu hiyo iliyosomwa jana na Jaji Lameck Mlacha aliyekuwa anasikiliza kesi hiyo, wakazi wa Mwanza watapata fursa ya kuuaga mwili wa hayati Mawazo leo kwenye viwanja vya Furahisha kabla ya kusafirishwa kesho kwenda Geita na hatimaye kuzikwa kijijini kwao Chikobe.

Akisoma hukumu ya kesi hiyo iliyofunguliwa na Mchungaji Charles Rugiko ambaye ni baba mdogo wa hayati Mawazo kupinga zuio lililowekwa na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, Charles Mkumbo, Jaji Mlacha alisema marehemu alikuwa na haki ya kufanyiwa ibada na kuagwa na wajibu wa dola ulikuwa kuandaa mazingira kuwezesha hilo kufanyika siyo kuzuia.

“Kazi ya dola ilikuwa kuandaa mazingira ili kuhakikisha haki ya mlalamikaji inakamilika,” alisema Jaji Mlacha.

Katika hukumu hiyo iliyosomwa kuanzia saa 7.35 hadi saa 8.05 mchana, Jaji Mlacha alitoa pia maelekezo kwa Kamanda Mkumbo azingatie haki ya asili, atoe ulinzi katika shughuli ya kuaga mwili wa Mawazo; na viongozi wa Chadema wajizuie kutoa kauli zitakazopandisha hisia za watu na uwanja wa kuaga mwili ili usigeuzwe kuwa wa siasa.

Kesi hiyo namba 11 ya mwaka 2015 ilifunguliwa Jumanne kupinga amri ya Kamanda Mkumbo ya Novemba 19 ya kupiga marufuku shughuli za kuaga mwili wa mwanaye aliyeuawa Novemba 14 na watu wanaodaiwa kuwa ni wafuasi wa CCM. Kamanda Mkumbo alipiga marufuku kwa madai ya kuwapo ugonjwa wa kipindupindu na sababu za usalama.

Mchungaji Mkumbo aliyeweka mawakili watatu wakiongozwa na John Mallya aliiomba Mahakama Kuu iondoe amri ya Kamanda Mkumbo kuzuia kuaga mwili wa Mawazo; itoe tamko kuwa zuio hilo ni batili na kinyume cha sheria na imkataze Kamanda Mkumbo kujihusisha na shughuli za mazishi na kuaga mwili huo.

Hata hivyo, katika hukumu hiyo, ambayo walalamikiwa walikuwa Kamanda Mkumbo na Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Jaji Mlacha alikubaliana na maombi mawili ya kwanza lakini akaelekeza ndugu na uongozi wa Chadema ngazi ya mkoa na Taifa, wakutane na Kamanda Mkumbo wapange jinsi ya kuaga mwili huo eneo watakalokubaliana ili atoe ulinzi lakini usiwe wa kupitiliza.

Hukumu yatolewa
Baada ya kupitia ushahidi wa maandishi na mkanda wa video uliowasilishwa na mlalamikaji na upande wa utetezi, Jaji Mlacha alisema: “Mahakama inayo nguvu ya kikatiba kufuta amri yoyote ambayo ni batili. Kifungu cha 19 cha Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kinazungumzia haki za binadamu, hivyo marehemu ana haki ya kuagwa na ndugu wana haki ya kumuaga ndugu yao.

“Kazi ya dola ilikuwa kuandaa mazingira ili kuhakikisha haki ya mlalamikaji inakamilika. Ni kweli upande wa Serikali haukupinga kuagwa kwa mwili wa Mawazo, bali ni namna ya uagaji. Lakini kutazama utu siyo vizuri kuongozwa na historia, hivyo nafikiri marehemu anastahili kuagwa Mwanza kwa kuwa baba yake mdogo yupo hapa,” alisema Jaji Mlacha.

“Kama polisi walikuwa na taarifa za usalama zinazoonyesha viashiria vya uvunjivu wa amani, haikuwa sahihi kutoa amri hiyo kwa sababu iliondoa haki ya kikatiba. Walichotakiwa kufanya ni kuwatafuta ndugu au viongozi wa Chadema na kushirikiana nao kuzungumzia suala hilo,” alifafanua Jaji Mlacha.

Aidha, Jaji Mlacha alisisitiza katika hukumu yake kwamba jambo la kuaga mwili na kwenda kuzika eneo jingine siyo geni nchini kwani limekuwa likifanyika maeneo mbalimbali hivyo marehemu anayo haki ya kikatiba kuagwa Mwanza. “Haki za binadamu haziwezi kuondolewa kwa urahisi na kwamba jamaa zake wa Chadema wa Mwanza nao walikuwa na haki ya kumuaga,” alisema.

Shangwe zalipuka
Tofauti na siku zilizopita, jana polisi hawakuonekana badala yake viwanja vya Mahakama vilitawaliwa zaidi na wafuasi wa Chadema. Baada ya kutolewa hukumu hiyo, kulikuwa na shangwe isiyo na kifani kwa ndugu, jamaa na wafuasi wa Chadema mkoani hapa ambao walifunga barabara inayopitia mahakamani hapo kutokea Kapripont, huku wakiimba “bado Wenje, bado Wenje” kuelekea kwenye Hoteli ya Gold Crest walikofikia viongozi wakuu wa chama hicho.

Ezekia Wenje alikuwa mbunge wa Nyamagana (2010/15) lakini aliangushwa katika uchaguzi mkuu uliopita na amefungua kesi katika Mahakama hiyo dhidi ya mshindi Stanslaus Mabula wa CCM.

Walivyosema
Mchungaji Rugiko alisema familia imefarijika na uamuzi huo ilhali Nuru Mawazo ambaye ni mke wa hayati Mawazo, akisema Mahakama imetenda haki na kwamba wanasubiri taratibu nyingine.

Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe alisema wanashukuru kwa uamuzi huo kwani haki imetenda. “Kwa sasa tunakwenda kwenye vikao kupanga taratibu za mazishi, kama Mahakama ilivyotuelekeza kukutana na kamanda wa polisi tutakutana naye, lakini hatutakubali kuonewa,” alisema Mbowe.

Kutoka Bunda, mwandishi wetu Christopher Maregesi ameripoti kuwa Mahakama ya wilaya imewafutia wafuasi watatu wa Chadema shtaka la unyang’anyi wa kutumia silaha walilokuwa wakikabiliwa nalo baada ya kutokuwapo kwa ushahidi wa kutosha.

Waliokuwa wakikabiliwa na shtaka hilo ni Gregory Juma (29) mkazi wa Mkuyuni mkoani Mwanza, Ibrahimu Issa (20) mkazi wa Mtaa wa Saranga wilayani humo na Lucas Andrea (30) mkazi wa Area “A” mkoani Dodoma.

Hakimu mkazi wa Mahakama hiyo, Ahmed Kasonso alisema jana kuwa licha ya upande wa mashtaka kuleta mahakamani hapo mashahidi wanne, ni mmoja tu aliyetoa maelezo yanayoendana na shtaka hilo huku wengine wakijikanganya. 


Alisema kuwa hali hiyo hailipi uzito wa kisheria shauri hilo kuendelea kuwapo mahakamani hapo, bali inatoa mwanya wa kuliondoa na hivyo kuwafanya washtakiwa hao wabakiwe na shtaka moja tu la wizi wa simu.CHANZO:MWANANCHI
Share on Google Plus

About mtanda blog

Blogger maarufu nchini Tanzania na mwanahabari mkongwe kwenye Tasnia ya habari
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments: