BannerFans.com

MBUNGE SUZAN KIWANGA AKWAMISHA KESI MAHAKAMANI MOROGORO

KATIBA YAKOLEZA KASI YA KUJIHAKIKISHIA URAIS KWA MAKADA WA CCM.


Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa.PICHA|MAKTABA

Dar es Salaam.
Siku chache baada ya Bunge Maalumu kupitisha Katiba Inayopendekezwa, mchuano wa urais ndani ya CCM umeshika kasi baada ya makada wanaowania nafasi hiyo kujihakikishia uzito wa madaraka wanayoyatafuta.

Mjadala wa Katiba ulikuwa umewaweka njiapanda makada hao, baadhi wakiwa wameshajitangaza na wengine wakijipanga chinichini, huku wakijiuliza wawanie urais upi; wa Muungano, Tanganyika au Zanzibar (kwa Wazanzibari), lakini sasa ni kama wamefunguliwa njia.


Hata hivyo, utaratibu wa watu kujitokeza licha ya kwamba ni haki yao, umekosolewa ukielezwa kuwa kama hakutakuwa na sifa maalumu, mchakato huo unaweza kumalizika kwa kupata mgombea asiyestahili.


Wengi wa makada wanaojitokeza na kutajwa ambao gazeti hili limewahi kuzungumza nao katika mahojiano maalumu, walionyesha wazi kuunga mkono serikali mbili dhidi ya tatu zilizokuwa zimependekezwa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba chini ya Jaji Joseph Warioba.


Ingawa baadhi yao hawakutaka kuweka bayana, habari zilizobainika katika makundi yanayowaunga mkono ni kuwa walikuwa wanaona serikali tatu zingeondoa madaraka makubwa aliyonayo Rais wa Muungano wa sasa katika muundo wa serikali mbili.


Jambo jingine lililokuwa linawakatisha tamaa makada hao ni hoja ya kutaka madaraka ya Rais yapunguzwe kwa kiwango kikubwa, iwapo ingepita ingeweza kuwakosesha uwezo wa kulipa fadhila kwa wanaowaunga mkono.


“Unadhani nani angetaka kuwa Rais wa Tanzania Bara pekee au awe Rais wa Muungano asiyekuwa na mamlaka Bara,” alisema kada kundi la mmoja wa wagombea.


Kutokana na hofu hiyo, nguvu za wagombea hao zilielekezwa kwanza kwenye Katiba ili kuhakikisha madaraka wanayoyasaka yanalindwa, ndipo waanze upya mchuano.


Taarifa zilizochapishwa kwenye vyombo vya habari juzi kuwa makundi ya wagombea yalikuwa yanapishana Dodoma kugawa fedha kushawishi uungwaji mkono wa wajumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC), zinaelezwa kuwa ni sehemu ya mchuano huo kushika kasi upya.


Kulikuwa na taarifa kuwa ingeibuliwa hoja ya kutaka wagombea wengine wabanwe na chama kwa kupiga kampeni, zaidi ya lile kundi la makada sita waliokwishapewa onyo kali na chama hicho.


Makada waliopewa onyo hilo ni mawaziri wakuu wa zamani, Edward Lowassa (61) na Frederick Sumaye (64) na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe (61).


Wamo pia Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Uhusiano na Uratibu), Stephen Wasira (69), Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, January Makamba (40) na aliyewahi kuwa Waziri wa Nishati na Madini, William Ngeleja (47).


Wana-CCM wengine wanaotajwa kuwania nafasi hiyo ni Waziri Mkuu Mizengo Pinda (66), Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Samuel Sitta (72), mbunge wa Nzega, Dk Hamis Kigwangalla (39), Naibu Waziri wa Fedha, Mwigulu Nchemba (39) na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Kazi Maalumu), Profesa Mark Mwandosya (65).


Pia yumo mbunge wa Songea Mjini, Dk Emmanuel Nchimbi (43), Rais wa Zanzibar, Dk Ali Mohamed Shein (66), Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano, Dk Mohamed Gharib Bilal (69) na Waziri wa Sheria na Katiba, Dk Asha-Rose Migiro (58).


Haki kuonyesha nia
Akizungumzia mbio hizo za urais kwa upande wa CCM na vyama vya upinzani, aliyekuwa makamu mkuu wa Chuo cha Mt. Augustino Mwanza (Saut), Dk Charles Kitima alisema walioonyesha nia na wanaotajwa wana haki kikatiba ya kuongoza nchi.


Alisema pamoja na kwamba wanaojitokeza wana haki, utaratibu unaotumika sasa haueleweki tofauti na miaka ya nyuma, vyama ndivyo vilivyokuwa vinapendekeza watu watakaogombea.


Alisema utaratibu huo unaonyesha kuwa nchi inakosa sifa ya viwango vya juu vya urais kwa kuwa kujitokeza kwa wingi huo kunazua maswali mengi na inatia wasiwasi.


Dk Kitima alisema ni lazima kuwe na sifa ya urais kwani atasaidia kwa watu kutokujitokeza au kujitokeza kama ilivyo sasa.


Alisema: “Viongozi wengi wanatafuta urais kwa ajili ya uchumi wa familia zao badala ya Taifa, hivyo wananchi lazima waeleweshwe.”MWANANCHI
Share on Google Plus

About mtanda blog

Blogger maarufu nchini Tanzania na mwanahabari mkongwe kwenye Tasnia ya habari
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments: